BLOGGER TEMPLATES AND TWITTER BACKGROUNDS »

www.thazealottz.blogspot.com

Promo

Saturday, November 26, 2011

Ray C azamia Kenya, apata mpenzi mpya

LINAPOTAJWA jina, Ray C, si rahisi kwa shabiki yeyote wa muziki ndani ya Afrika Mashariki, moja kwa moja fikra zake zitahamia kwa malkia wa muziki kutoka Tanzania mwenye vibao vya kusisimua, sauti na sura ya kuvutia.

Rehema Chalamila, kwa jina lake halisi, amekuwa jijini Nairobi kwa takribani miezi minane sasa akiendelea na shughuli zake na amesisitiza kwamba hajachuja kimuziki.

Nusura vyombo vya habari vinirudishe chini mwaka jana, lakini ninashukuru Mungu kwamba nilihimili yote na sasa ninajiendeleza kisawasawa kwenye muziki, anasema mwimbaji huyo katika mazungumzo yake na Mwanaspoti yaliyofanyika jijini Nairobi.

Akiwa jijini hapa, Ray C, ametoa vibao kadhaa kikiwamo cha Moto Moto alichokitoa akishirikiana na msanii chipukizi wa hapa Kenya, French Boy.

Ray C anasema kibao hicho ni sehemu ya maandalizi ya albamu mpya anayoamini itakuwa kali zaidi kuliko kazi zake zote za awali.
Baadhi ya nyimbo zake za awali ni pamoja na Na Wewe Milele Wanifuatia Nini naUko Wapi.

Kwanini kaamua kupiga kambi Nairobi
Anasema ni kwa sababu Wakenya wamekuwa wakimpa sapoti ya kutosha tangu alipoanza shughuli za muziki.

Kupitia kwa mashabiki wa Kenya, nimepiga hatua kubwa na kwa kweli sitaondoka Nairobi hivi karibuni.

Na hivi karibuni mtasikia habari kwamba nimeolewa hapa hapa, anasema Ray C huku akimwaga tabasamu la haja.
Alipoulizwa iwapo tayari amepata mchumba Mkenya, Ray C alikataa kutoa ufafanuzi wa kutosha, akisisitiza kwamba hiyo itakuwa mada ya wakati mwingine.

Uchumba wake uliovunjika Tanzania
Mwaka jana, Ray C, mwenye umri wa miaka 29 aliripotiwa kumtema mchumba wake ambaye pia ni mwanamuziki wa hip hop nchini kwake Tanzania, Lord Eyes.

Akizungumzia hilo, anasema: Eyes alikuwa mchumba wangu na tulishibana kimapenzi. Lakini tulitengana kutokana na tofauti ambazo hutokea baina ya wachumba, mambo haya huwatokea watu wengi tu.

Anasema tangu apige kambi jijini Nairobi anakopiga shoo kwenye klabu mbalimbali, amepiga hatua kubwa ikiwa ni pamoja na kupata fedha za kujenga nyumba kwao Tanzania pamoja na kumfungulia miradi mama yake.

Anasema anajua kuwa muziki ndiyo kazi yake na hivyo yuko tayari kukabiliana na changamoto zozote zinazojitokeza mbele yake.

Mimi kwanza ni mcha Mungu. Ninawasamehe wote ambao wamekuwa wakinipachika majina mbali na kueneza porojo chafu kuhusu mimi na muziki wangu, anasema Ray C ambaye macho yake ya kikombe na umbo la kuvutia huwatia kiwewe mashabiki wake.

Unajua unapokuwa nyota katika jamii, ni lazima watakuwapo watu wa kukufuata kwa maneno. Hata waandishi wa habari wataandika mambo tofauti yasiyo na ukweli, hufanya hivyo ili tu wauze magazeti.

Ray C, mkali pia kwa mitindo ya unenguaji jukwaani mwaka jana shoo yake ya mjini Nakuru nusura ivunjike dakika za mwishoni baada ya kudaiwa alitaka kuvua mavazi yake na ya shabiki mmoja wa kiume aliyepanda jukwaani.

Ndiyo ninachosema, hii ni gharama ya umaarufu. Sijakatishwa tamaa na uvumi ule kwani nilishawasamehe waliozusha, ndiyo maana nimerudi tena Kenya baada ya kualikwa na Kituo cha Maliza Umaskini,anasema dada huyo.

Akizungumzia zaidi muziki, anasema wote wanaodhani kuwa amefifia, sasa wakae mkao wa kula. Nakuja na albamu ya tano itakayokuwa na nyimbo 12.

Yeyote anayedhani kwamba nimekwisha kimuziki, anapasa kutafakari tena. Jina Ray C liko juu na haliwezi kumalizwa na porojo.

Anazitaja baadhi ya nyimbo zilizoko kwenye albamu yake ya Moto Moto kuwa ni pamoja na Itakuwaje, Mama Ntilie na huo unaobeba jina la albamu.

Ugomvi na Promota wake
Mwaka jana alikorofishana na Promota Sadat (anayemiliki Maliza Umaskini) na ilidaiwa Lord Eyes ni mmoja wa watu waliochangia katika kutoelewana kwake na mapromota Wakenya.

Hapana si kweli. Nilikosana na Sadat katika hali ya kawaida na wala Eyes hakuchangia. Kwanza yeye alitaka niinuke kibiashara na kimuziki,anasema.

Lakini kwa sasa nimemsahau Eyes na nimeanza maisha mapya kimuziki na kijamii vilevile. Kibinadamu nataka pia mchumba ili ikiwezekana nianzishe familia yangu. Sitakuwa mpweke milele.

Uhusiano wake na Kikwete
Rais wa Tanzania, Rais Jakaya Kikwete ni mmoja wa mashabiki wangu wakubwa. Ndiyo maana hata alipenda muziki wangu utumike kwenye kampeni zake mwaka jana, ni ushahidi wa ubora wa kazi zangu, hazipendwi na vijana tu,anasema kwa kujiamini. 




Kwanini huimba mapenzi zaidi
Asikwambie mtu bwana. Mapenzi ndiyo kila kitu. Pasipokuwa na mapenzi, hakuna familia, hakuna maelewano. Mapenzi huvuta hisia za kila mtu, awe mzee au kijana, wote wanataka kusikiliza na kuhisi mapenzi. Hii ndiyo sababu yangu ya kuimba mno kwa nyimbo za mapenzi,anasema.

Mashabiki wake wa Tanzania
Mimi ni mwanamuziki wao, kule ni nyumbani. Wanivumilie tu nitaenda japo kwa sasa nimejikita zaidi Nairobi, lakini waendelee kuzipenda kazi zangu kama zamani, anawaambia Watanzania


Monday, November 21, 2011

Aslay abadili uchumi wa familia


WAKATI wasanii wengi wa muziki wakiishia kufanya matanuzi kwa fedha za mapato ya kazi zao, kinda wa anayetamba na wimbo wa Nakusemea, Aslay Isihaka, ameamua kubadili maisha ya familia yake kwa kumpa mama yake mtaji mkubwa wa biashara.

Kinda huyo anayechipukia katika muziki wa kizazi kipya, amesema ameamua kufanya hivyo kutokana na ukali wa maisha uliokuwa ukiiandama familia yake.

Kuna wakati tulikuwa tunalala na njaa, sasa hatutalala njaa tena, alisema msanii huyo anayesoma Kidato cha Kwanza katika Shule ya Sekondari Tandika.

Nilikuwa naumia sana na kumwonea huruma mama yangu, lakini naimani sasa haya yote yamekwisha.

Aslay ni kati ya watoto wanaolelewa katika kituo cha Mkubwa na Wanawe, kinachomilikiwa na Saidi Fela, mmiliki wa kikundi cha TMK Wanaume Family.

Kituo hiki kipo maeneo ya Temeke-Mwembe Yanga, Dar es Salaam.